1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kenya na Somalia zafungua ukurasa mpya wa ushirikiano

Thelma Mwadzaya7 Mei 2024

Kenya na Somalia zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baada ya waziri mkuu wa Somalia Hamza Abdi Barre kufanya ziara rasmi na kupokelewa na naibu wa rais wa Kenya Rigathi Gachagua.

https://p.dw.com/p/4fb24
Mkutano wa viongozi wa kikanda mjini Mogadishu
Somalia iko mstari wa mbele kutangamana na washirika wapya baada ya kujiunga rasmi na jumuiya ya Afrika Mashariki.Picha: Ethiopian PM Office

Somalia iko mstari wa mbele kutangamana na washirika wapya baada ya kujiunga rasmi na jumuiya ya Afrika Mashariki. Ziara ya leo inafanyika baada ya kikao cha tatu cha pamoja cha ushirikiano. Wakati huo huo, Kenya imeimarisha mkakati wake wa kupambana na ugaidi hususan wafadhili ukizingatia kitisho cha Al Shabaab.

Soma pia: Somalia yajiunga rasmi na Jumuiya ya Afrika Mashariki

Kikao hicho cha kihistoria,kilifanyika kwenye makaazi rasmi ya naibu wa rais Rigathi Gachagua katika eneo la Karen. Waziri mkuu wa Somalia Hamza Abdi Barre aliyewasili Nairobi siku ya Jumatatu, alipokelewa na waziri kiongozi na wa mambo ya kigeni wa Kenya, Musalia Mudavadi. Ajenda ya kikao ilijikita kwenye ushirikiano wa pamoja wa kidiplomasia na kibiashara.

Kwanini Al-Shabab inawatia hofu wasomali?

Kwa upande wake, naibu wa rais wa Kenya Rigathi Gachagua ameusisitizia umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa pamoja na majadiliano.Kikao hiki kinafanyika baada ya mkutano wa tatu wa pamoja uliowaleta mawaziri wa pande zote kwenye meza ya mazungumzo tarehe 3 hadi 6 mwezi huu huu wa Mei.

Viongozi hao wameahidi kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na umuhimu wa kusuluhisha migogoro kwa amani. Wakati huo huo, kitisho cha ugaidi kutokea wapiganaji wa Al Shabaab kimepata pigo jipya baada ya Kenya kuimarisha mkakati wake unaowalenga wafadhili. Kwenye mkutano maalum wa Jumatatu wiki hii, waziri wa usalama wa taifa Kithure Kindiki alibainisha kuwa wako imara na watakabiiana na yeyote anayefadhili ugaidi kwa njia za kinyemela.Kenya na Somalia zinafanyia kazi masuala ya pamoja ya kupambana na ukame,njaa na migogoro.